Katika kuendelea kutekeleza maagizo hayo ya Serikali ya kupokea malipo kwa njia ya kieletroniki ili kuhakikisha pia tunaendana na muda uliotolewa, Jeshi la Polisi kuanzia tarehe 8/05/2019 lilianzisha mfumo wa kukusanya malipo kwa ajili ya kulipia taarifa ya kupotelewa mali ( Loss Report) kwa Mikoa ya Dar es Salaam na Pwani.
Mfumo huu ulioanzishwa na Jeshi la Polisi utamwezesha mwananchi kutoa taarifa za upotevu wa mali au nyaraka kwa kupitia mtandao na kuweza kupata loss report bila kufika Kituo cha Polisi, isipokuwa kwa anayetoa taarifa ya upotevu wa kitabu cha kumiliki silaha, kadi ya gari, hati ya kiwanja au shamba, huyu itamlazimu kufika kituo cha Polisi. Mwananchi anaweza kutoa taarifa ya kupotelewa mali au nyaraka kwa kutumia kompyuta au simu yenye internet.
Taarifa hiyo inaweza kutolewa akiwa mahali popote pale ilimradi awe na kifaa cha kieletroniki chenye internet atakachotumia kutolea taarifa. Ili kutoa taarifa bila kufika kituoni inambidi mwananchi kutembelea tovuti ambayo nimeitaja awali ambayo ni https://lormis.tpf.go.tz inayopatikana kwa lugha ya Kiswahili na Kiingeleza. Akishaingia kwenye tovuti atabonyeza kitufe cha “ S a jili M a li I li y o p o t e a ” na ataendelea kujaza fomu atakayoipata. Baada ya kujaza fomu hiyo atatakiwa kufanya malipo.
Mfumo huu wa malipo wa Loss report unaowawezesha wananchi kulipa malipo hayo kupitia mfumo wa kieletroniki yaani Government electronic Payment Gateway (GePG) unapatikana kwenye mitandao yote ya simu na kwenye mabenki. Mwananchi anapojaza fomu ya Loss report kwenye mtandao atapata namba ya malipo (Control number) ambayo kupitia tovuti hiyo ya Polisi inaanzia na 99108 na kuendelea / kufuatiwa na namba nyingine.
Kwa wale wananchi waliopoteza laini za simu, kadi za benki au vitambulisho na kujaza maombi yao kwa kutumia kadi zao za NIDA au namba ya NIDA hawahitajiki kwenda Kituo cha Polisi kwani mfumo huu wa Loss report umeunganishwa na mfumo wa NIDA ambao una uwezo wa kuthibitisha taarifa za vitambulisho hivyo moja kwa moja (online).Kwa maana hiyo mwananchi mwenye kitambulisho cha NIDA au namba na akawa amepoteza laini za simu ana uwezo wa kujaza fomu online na kupata loss report yake online.
Aidha, wengine wanaotakiwa kufika kituoni ni wale waliopoteza mali zikiwemo vitabu vya kumiliki silaha, kadi za gari na hati za nyumba au mashamba hizi zinahitaji uchunguzi wa Polisi ufanyike kabla ya Loss Report haijatolewa kwa mhusika. Pia ambao wanatakiwa kuendelea kutoa taarifa zao katika vituo vya Polisi ni wale ambao hawana simu au kompyuta zenye internet itakayowezesha kutoa taarifa ya kupotelewa na mali au nyaraka kwa njia ya mtandao (online).
Kwa wananchi wa aina hii Wakuu wa Vituo na Wahasibu wameshapata mafunzo na maelekezo ya namna ya kuwahudumia. Mfumo huu wa kulipia kwa ya njia ya mtandao (online) na kupata loss report kama nilivyosema tulianza na Mikoa ya Dar es Salaam na Pwani, napenda kuwajulisha kuwa mfumo huu unatumika kwa nchi nzima sasa. Hivyo ninapenda kuwapa taarifa watoa huduma za mawasiliano kuwa kuanzia sasa wawape huduma wananchi wote wanaofika kwao wakiwa na Loss report ya kieletroniki.
Watoa huduma pale watakapokuwa na mashaka wanaweza kuthibitisha/ kuhakiki kama Loss report ya mwananchi ni halali au ya kugushi kwa kutumia njia mbili:- Njia ya kwanza ni kutembelea tovuti ya loss report ya Jeshi la Polisi ambayo ni https://lormis.tpf.go.tz na kwenda kwenye kitufe cha “Angalia Ripoti yako” hapo ataingiza namba ya malipo (Control Number) ambayo atapewa na mwananchi pamoja na namba ya kitambulisho chake, ripoti ikitoka itakuwa ni sahihi na isipotoka itakuwa ni ya kughushi.
Njia ya pili, kwa wale watoa huduma ambao wana mifumo ya kieletroniki na wangependa kujiunga na mfumo huu tunatoa Application Program Interface (API) ambayo itaweza kuwaunganisha na hapo wataweza kuwahakiki wateja wao kwa njia ya kieletroniki bila ya kufika au kutembelea tovuti yetu.
Imetolewa na: David A. Misime – SACP
Msemaji wa Jeshi la Polisi Makao Makuu ya Polisi.