TIMU ya Tanzania Bara, Kilimanjaro Stars imepangwa katika Kundi C pamoja na Zanzibar, Kenya na Djibouti katika Mashindano ya Kombe la Chalenji kwa timu za wanaume.
Ratiba ya mashindano hayo, ambayo yatafanyika Kampala, Uganda kuanzia Desemba 7-18, ilipangwa jana jijini Dar es Salaam na kutangazwa na Katibu Mkuu wa Baraza la Soka la Afrika Mashariki (Cecafa), Nicolaus Musonye.
Hii ni mara ya pili kwa Tanzania Bara kupangwa pamoja na Zanzibar, kwani katika michuano ya wanawake ya Cecafa inayomalizika leo jijini Dar es Salaam, katika hatua ya makundi, timu hizo zilikuwa pamoja katika Kundi A, lakini Zanzibar ilitolewa mapema.
Kwa mujibu wa ratiba hiyo, Kundi A linaundwa na wenyeji Uganda ambao watakuwa pamoja na Ethiopia, Eritrea na Burundi wakati Kundi B linaundwa na timu mualikwa ya DR Congo, Sudan Kusini, Ethiopia, Burundi na Sudan.
Mbali na ratiba hiyo ya wakubwa, Cecafa pia jana ilipanga ratiba ya makundi kwa timu za wasichana wenye umri chini ya miaka 17, ambayo mashindano yake yatafanyikia Jinja, Uganda pia.