Mamlaka ya Hali ya Hewa nchini Tanzania (TMA) imetangaza kuwa Kimbunga Kenneth kimeongezeka kasi na kinatarajiwa kufika pwani ya kusini ya Tanzania na kaskazini mwa Msumbiji kuanzia usiku wa Alhamisi wiki hii.
Kwa mujibu wa TMA, mpaka sasa (Jumatano mchana) kimbunga hicho kipo kilomita 450 kutoka pwani ya Mtwara na kina kasi ya kilomita 130 kwa saa.
Kufikia usiku wa leo, Aprili 24 kimpunga hicho kitakuwa kilomita 250 kutoka pwani ya Mtwara, kikiwa kinasafiri kwa kilomita 150 kwa saa.
Kimbunga hicho kinatarajiwa kuongeza nguvu zaidi Alhamisi mchana ambapo kitakuwa kinasafiri kwa kilomita 170 kwa saa na kitakuwa kilomita 150 kutoka pwani ya Mtwara.
Kwa mujibu wa TMA, eneo husika ambalo kimbunga hicho kitatua (landfall) litakuwa nchini Msumbiji, kikiwa na kasi ya kilomita 100 kwa saa. Eneo hilo litakuwa kilomita 200 kutoka pwani ya Mtwara.
Hata hivyo, mkoa wa Mtwara na maeneo jirani hususani mikoa ya Lindi na Ruvuma yataathirika pakubwa (athari zinategemewa kufikia umbali mpaka wa kilomita 500 kutoka Mtwara).