Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amemuagiza Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu Sera na Uratibu, Bibi Jenista Mhagama akutane na mawaziri wa sekta nyingine na watafute namna ya kuondoa mkanganyiko uliopo kwenye vyombo vya udhibiti hapa nchini.
Waziri Mkuu ametoa agizo hilo Bungeni jijini Dodoma, kwenye mkutano wa 15 wakati akihitimisha hoja ya bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu, taasisi zake na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2019/2020.
Amekuwa akitoa ufafanuzi juu ya masuala yaliyogusa vyombo vya udhibiti kama vile Mamlaka ya Chakula na Dawa TFDA, Shirika la Viwango Tanzania TBS, Mkemia Mkuu wa Serikali, Mamlaka nyingine za udhibiti pamoja na Mamlaka ya Mapato Tanzania TRA, OSHA, BRELLA na Taasisi ya Mionzi ambayo yaligusiwa na Waheshimiwa Wabunge.
Amesema licha ya Serikali kujenga mazingira wezeshi na rahisi ya kufanya biashara na uwekezaji, bado kumekuwepo na malalamiko kutoka kwa wafanyabiashara na wawekezaji kama walivyoeleza Waheshimiwa Wabunge wakati wa kuchangia hoja hiyo.