Zimebaki siku nne kwa rai wa Jamuhuri ya Kidemokrasi ya Congo (DRC) kumchagua mtu atakayerithi mikoba ya Joseph Kabila.
Wagombea watatu ndio wanaotajwa zaidi na ni vigumu hata kudhani kuwa wanaowania kiti hicho wapo zaidi ya ishirini na mmoja wao ni mwanamke.
Bi Marie-Josee Ifoku yupo kwenye kinyang’anyiro cha kurithi Ikulu ya Kinshasa kutoka kwa Kabila akichuana na Emmanuel Ramazani, Martin Fayulu na Felix Tshisekedi ambao ndio wanaouvuma zaidi.
Bi Ifoku, mwenye miaka 53 ni mama wa watoto nane si mgeni katika siasa. Alishawahi kuwa naibu gavana wa jimbo la Tshuapa kwa miezi sita mwaka 2016 kabla ya kuchaguliwa kuwa gavana wa jimbo hilo kuanzia Oktoba 2016 mpaka Oktoba 2017.
Bi Ifoku anasema kipaumbele chake cha kwanza kitakuwa kufanya mabadiliko ya katiba ili kuhakikisha haki za kiraia zinalindwa na njia ya maendeleo inaandaliwa.
Tatizo la vita limekuwa donda ndugu nchini DRC na bi Ikofu amesema atatumia uwezo wake wote kulishughulikia
Mgombea huyo wa urais amesema ameshangazwa kwa wingi wa simu za watu ambao wamekuwa wakimpongeza na kumhimiza wakimwambia kumekuwa na uongozi wa wanaume kwa miaka 58 lakini hawaoni mabadiliko yoyote muhimu.
Wakati huohuo, Mke wa rais anayemaliza muda wake Joseph Kabila bi Olive Lembe Kabila ametaka wanawake wasiwapigie kura viongozi mabao hawajaoa wanawake wa Congo.