Mwendesha mashitaka mkuu wa Saudi Arabia Saud al-Mojeb amesema mauaji ya mwandishi wa habari Jamal Khashoggi yalipangwa. Taarifa hii inakinzana na iliyotolewa awali kwamba Khashoggi aliuawa kwa bahati mbaya akiwa kwenye ubalozi mdogo wa Saudia Arabia, nchini Uturuki. Maafisa wa Saudi Arabia awali walidai kwamba Khashoggi aliondoka ubalozini hapo. Kulingana na mwendesha mashitaka huyo taarifa hiyo iliyotolewa na Uturuki, inaashiria kwamba watuhumiwa wa mauaji ya Khashoggi walifanya kitendo hicho kwa kudhamiria. Msemaji wa Kansela wa Ujerumani Angela Merkel, amesema kwamba, kansela amezungumza na mwana mfalme wa Saudi Arabia Mohammed Salman na kulaani mauaji hayo. Aidha ametaka kufanyika uchunguzi wa haraka, wa wazi na wenye kuaminika na wahusika kufikishwa mbele ya sheria.