Mkoa wa Arusha umeenza kutekeleza Agizo la Waziri mkuu la kuanzishwa kwa kliniki maalumu kwenye hospitali za mikoa na wilaya kwa ajili ya kuondoa hatari ya waratibu wa dawa za kulevya kupata maambukizi ya ugonjwa wa ukimwi na vvu.
Akifungua semina ya siku moja ya wadau wa masuala ya mapambano na
udhibiti wa dawa za kulevya na Ukimwi Katibu Tawala wa mkoa wa Arusha Richard Kwitega, amesema kuwa mkoa upo tayari umetekeleza agizo hilo na umejipanga kuhakikisha unapunguza matumizi ya dawa za kulevya na mapya ya VVU.
Amesema kuwa Uanzishwaji wa Kliniki hizo za matibabu kwa watumiaji wa dawa za kulevya ni mkakati wa serikali ya mkoa kuhakikisha inatokomeza matumizi ya dawa za kulevya sanjari na maambukizi mapya ya vvu na kuwataka wadau kulipigia debe suala hilo popote.
Kwa Upande wake Kamishna wa dawa za Tiba wa mamlaka ya kudhibiti na kupambana na dawa za kulevya nchini Dkt.Peter Mfisi amesema kuwa zoezi hilo ,wamepanga kuhakikisha kuwa ifikapo mwaka 2020 hapa nchini asilimia 90 wanaifikia jamii katika kuhakikisha mapambano ya dawa za kulevya yanakuwa historia hapa nchini.
Amesema kuwa kwa mujibu wa umoja wa mataifa Tanzania imeonyesha kuwa imefanikiwa katika mapambano ya kudhibiti dawa aina ya Heroin kwa asilimia zaidi ya 90 hivyo wamejipanga kuhakikisha wanaendeleza mapambano sanjari na udhibiti wa dawa hizo.
Nae Dkt.Neema Makyao ambaye ni mwakilishi wa wizara ya Afya akitoa mada amesema kuwa hali ya maambukizi nchini ikionyesha kupungua kuna makundi baadhi ya maeneo likiwemo la watumiaji dawa za kulevya kwa njia ya kujidunga yapo hatarini kupata magonjwa nyemelezi ikiwemo ukimwi na kifua kikuu.
Amesema serikali kupitia wizara ya Afya imejipanga na kuweka mazingira wezeshi katika utoaji huduma za vvu na ukimwi kwa lengo la kupunguza maambukizi kwa kuelimisha jamii ambapo asilimia 90 ya watu wanaoishi na vvu na kujitambua hali zao ifikapo mwaka 2020 wanajitambua na kuongeza hali za kutumia dawa za kufubaza makali ya vvu.