Mkutano wa kilele wa wakuu wa nchi zilizoendelea kiviwanda na zenye uchumi unaoinukia, G20 unaingia siku yake ya pili na ya mwisho hii leo nchini Argentina, huku wanadiplomasia wakisaliwa na masaa machache ya kuondoa mgawanyiko wa masuala makubwa ikiwemo biashara ya dunia, mabadiliko ya tabia nchi na uhamiaji. Siku ya leo pia itashuhudia mkutano unaotazamiwa baina ya rais wa Marekani Donald Trump na mwenzake wa China Xi Jinping, ambao mataifa yao yamekuwa katika vita vya kibiashara, ambapo ushuru mpya wa Marekani kwenye bidhaa za China utaanza kutumika mwezi mmoja kuanzia sasa. Wakati huo huo, viongozi wawili wanaokabiliwa na ukosoaji wa mataifa ya Magharibi -Rais wa Urusi Vladimir Putin na Mwana Mfalme wa Saudi Arabia Mohammed bin Salman – walionekana kuwa karibu na kuketi meza moja kwa mazungumzo. Wasiwasi wa usalama ni suala ambalo limegubika mkutano huo wa siku mbili, ambapo jumla ya mabomu manane ya petroli yaligunduliwa na maandamano yakitawala nje ya mkutano huo.