RAIS Yoweri Museveni ameyaambia makundi ya kisiasa nchini Uganda kuwa umasikini ni janga kubwa nchini humo ambalo linapaswa kupigwa vita kwa moyo wa dhati badala ya kuleta siasa ambazo hazina tija.
Kiongozi huyo aliyasema hayo mjini Kasese akiwa katika ziara nchi nzima ya kuhamasisha wananchi kujitafutia mali na kuondokana na umasikini. Alisema kitendo cha wanasiasa wa upinzani kubeza juhudi za kupiga vita umasikini katika vyombo vya habari ni undumilakuwili wa kisiasa ambao unaonesha ni kwa namna gani wametanguliza masilahi binafsi mbele na si maslahi ya wananchi.
“Watu wanaojiita wanasiasa wa upinzani wanapaswa kujua hali za watu wetu na hali wanazopitia ili waweze kuwasaidia watoke hapo walipo kwa kuwainua kwa mawazo chanya yatakayowawezesha kupiga teke umasikin.”
“Ni mawazo mgando yasiyokuwa na maana yoyote ile kwa wanasiasa wa upinzani kusema wanasubiri mpaka serikali iliyopo madarakani iondoke ndipo wataanza kutoa mbinu kwa wananchi kuondokana na umasikini,” alisema.
Rais Museveni alisema hakuna cha serikali wala upinzani linapokuja suala la umasikini kwa watu wa Uganda. “Mtu makini hawezi kuchanganya siasa na uhalisia wa maisha ya watu, viongozi wote mnatakiwa kuwafuata wananchi na kuwasaidia kuondoa umasikini katika nyumba zao,” alisema.