Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Angeline Mabula,amelitaka Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) kuhakikisha linajenga majengo yenye ubora katika miradi mbalimbali inayopewa kujenga nchini.
Dkt Mabula ametoa kauli hiyo wakati wa ziara ya kukagua mradi wa ujenzi wa ofisi ya Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania Kanda ya Ziwa (TFS),eneo la Mkolani jijini Mwanza akiwa katika ziara yake ya kuangalia utendaji kazi wa sekta ya ardhi katika Kanda ya Ziwa pamoja na kukagua miradi ya ujenzi inayofanywa na Shirika la Nyumba la Taifa (NHC).
Amesema,ni vyema shirika hilo likahakikisha miradi yoyte inayopewa ya ujenzi inakuwa na viwango na kuepuka udanganyifu wowote unaoweza kufanyika kama vile kuweka kiwango kidogo cha saruji katika ujenzi, jambo linaloweza kusababisha majengo yasiyo na ubora.
Amewataka wafanyakazi wa mradi wa ujenzi wa jengo la TFS mkoani Mwanza kuwa waaminifu wakati wote wa ujenzi ili kuepuka sifa mbaya ya udokozi inayoweza kusababisha shirika la Nyumba kukosa kazi nyingine,kwa kujenga majengo yaliyo chini ya kiwango.
Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi amelisifu shirika la Nyumba la Taifa (NHC) kwa kufanya kazi vizuri katika ujenzi wa Ofisi na nyumba za watumishi,na kulitaka shirika hilo kuhakikisha inakamilisha ujenzi wa majengo yake katika kipindi kifupi kwa kuwa linahitaji kufanya kazi usiku na mchana.
Meneja wa Shirika la Nyumba la Taifa mkoa wa Mwanza Fadhili Ntahena,amesema, ujenzi wa jengo la Ofisi ya Wakala wa Huduma za Misitu (TFS) Kanda ya Ziwa unaosimamiwa na shirika lake unagharimu zaidi ya shilingi Bilioni 1.5,na ulianza Septemba mwaka huu ikiwa ni sehemu ya miradi mbalimbali ambaloShirika hilo limepewa na serikali kuijenga.
Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi wa Ubunifu wa Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) Magreth Ezekiel amesema NHC imejipanga katika miradi yake mbalimbali iliyokabidhiwa na mipango ya Shirika ni kuhakikisha miradi yote inakamilika ndani ya miezi sita,na mradi wa ujenzi wa jengo la TFS Mkolani.