Arusha
Serikali imeshauriwa kuona umuhimu wa kuongeza bajeti ya maendeleo katika sekta ya kilimo kutoka asilimia 2 ya sasa kukidhi azimio la Malabo na Maputo linalizitaka serikali kutenga asilimia 10 kwenye sekta ya kilimo ili kuongeza mchango wa sekta hiyo kuchangia katika pato la taifa na usalama wa chakula.
Pia imepongezwa kwa dhati kwa mikakati yake na jitihada kubwa katika kuendeleza na kuboresha mazingira mazuri ya uwekezaji katika sekta ya kilimo nchini katika kufikia azma ya mapinduzi ya viwanda.
Katika hatua za awali kutekeleza azma hiyo serikali imefuta na kupunguza ada na tozo 54 zinazotozwa na wizara idara na taasisi zinazojitegemea ili kuondoa kero na urasimu kwa wafanyabiashara na kuboresha mazingira ya biashara.
Akiongea na vyombo vya habari jijini Arusha wakati akichambua bajeti ya serikali hususani kwenye sekta ya kilimo Mwenyekiti wa baraza la taifa la kilimo ,Jackline Mkindi ambaye pia ni Mkurugenzi wa TAHA alisema kuwa kwa misingi hiyo ukuaji wa uchumi umekuwa kwa asilimia 7.0 mwaka 2018 kulinganishwa na mwaka 2017 kwa asilimia 6.3.
Amesema kuwa pato la taifa limefikia trillion 129.4 kwa mwaka 2018 ikilinganishwa na shilingi trillion 118 mwaka 2017 na kilimo kinachangia katika pato la taifa asilimia 28.2 hivyo uwekezaji mkubwa unahitajika
Kwa mujibu wa Mkindi uboreshaji wa mazingira mazuri ya kilimo biashara katika kuimarisha mazingira mazuri ya kilimo nchini hotuba hiyo ya waziri wa kilimo imeonyesha kuwekeza nguvu zaidi mpango kazi wa kuboresha mazingira ya biashara katika sekta ya kilimo ili mazingira yawe rafiki na na yenye gharama nafuu.