Mbunge wa Mbeya Mjini, Joseph Mbilinyi ‘Sugu’ na Katibu wa Chadema Kanda ya Nyanda za Juu Kusini, Emmanuel Masonga wamepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya wakikabiliwa na shtaka la kutumia lugha ya fedhea dhidi ya Rais John Magufuli.
Wakili wa Serikali, Joseph Pande amedai mahakamani hapo, kuwa washtakiwa hao walitenda kosa hilo Desemba 30 mwaka jana katika viwanja vya Shule ya Msingi Mwenge.
Wakili Pande amesema upelelezi wa shauri hilo umekamilika na wapo tayari kuendelea usikilizwaji kadiri Mahakama itakavyoona.
Hata hivyo, wakili anayewatetea Sugu na Masonga, Wakili Sabina Yongo ameiomba mahakama hiyo kuwapa muda kwani shauri hilo ndio limefikishwa mahakama hapo kwa mara ya kwanza hivyo anahitaji muda wa kukaa na wateja wake kwanza na aliiomba mahakama hiyo kuwapatia dhamana.
Lakini wakili wa Serikali, Pande ameiomba mahakama hiyo kutowapatia dhamana washtakiwa kwa madai kwamba ni kwa usalama wao.
Hakim mkazi mfawidhi wa mahakama hiyo, Michael Mteite amesema uamuzi wa dhamana kwa washtakiwa hao atatoa Ijumaa ya wiki hii na kuamuru wapelekwe mahabusu.