Rais Donald Trump wa Marekani amemfuta kazi mkurugenzi wa shirika la usalama na miundombinu ya mtandao, kwa kukosowa kauli yake juu ya wizi wa kura kwenye uchaguzi wa Novemba 3. Trump ametumia akaunti yake ya Twitter kumfukuza kazi Christopher Krebs, akisema kauli yake ya hivi karibuni kutetea usalama wa uchaguzi ilikuwa si sahihi hata kidogo. Kufukuzwa kwa Krebs kunakuja wakati Trump akiendelea kukataa kuyatambuwa matokeo ya uchaguzi huo ambao mpinzani wake mkuu kutoka chama cha Democrat, Joe Biden, alishinda. Krebs si afisa wa kwanza anayeshuku madai ya Trump kufutwa kazi. Mnamo tarehe 9 Novemba, alimfukuza kazi Waziri wa Ulinzi Mark Esper katika juhudi za kuweka watu wanaomtii kwenye nafasi za juu ya wizara hiyo. Krebs ndiye aliyekuwa akiliongoza shirika hilo la usalama wa mitandaoni tangu lilipoanzishwa mara tu baada ya uchaguzi wa 2016, ambao ulitajwa kuingiliwa na Urusi.