Rais wa Marekani Donald Trump amesema jana kwamba ataondoka ikulu ya White House baada ya rais mteule Joe Biden kuthibitishwa rasmi mshindi wa uchaguzi, na kurudia kwamba hatakiri kuwa ameshindwa uchaguzi huo.Alipoulizwa na waandishi wa habari kama ataondoka White House iwapo kamati ya wajumbe maalumu maarufu Electoral College itathibitisha ushindi wa Biden, Trump alikiri kuwa ataondoka, ingawa alisema iwapo wajumbe hao watamthibitisha watakuwa wamefanya kosa na kuongeza kuwa itakuwa vigumu kukubali. Amerudia madai yake kwamba kulikuwa na udanganyifu kwenye uchaguzi huo, ingawa kwa mara nyingine hakuweza kuthibitisha madai yake. Kwenye mkutano na waandishi wa habari katika kuadhimisha sherehe za Siku ya Shukrani, Trump alifikia hatua ya kuifananisha miundombinu ya uchaguzi wa Marekani na ya mataifa ya ulimwengu wa tatu.