Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Hamisi Kigwangalla, ameuagiza uongozi wa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro, uwaruhusu wananchi wa Kata ya Alaitole wajenge shule ya wasichana ya bweni katika eneo la Esere ,lililo ndani ya Mamlaka hiyo, ili waweze kupata elimu.
Ametoa agizo hilo kufuatia wananchi hao kuzuiwa kwa muda mrefu kutekeleza mradi huo, na kuutaka uongozi wa Mamlaka hiyo utoe kibali cha kuwawezesha wananchi kata hiyo, kuanza ujenzi haraka iwezekanavyo ili fedha zilizotolewa na Serikali shilingi milioni 298, zianze kutumika.
Dkt. Kigwangalla ametoa maagizo hayo alipokuwa akizungumza na kusikiliza kero za wananchi wa Kata Alaitole wilayani Ngorongoro ,kwenye mkutano wa hadhara uliowashirikisha viongozi wa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro, viongozi wa serikali wa kata hiyo, viongozi wa mila wa kabila la Masai, madiwani na Mbunge wa jimbo la Ngorongoro Mhe. William Ole Nasha.
Hata hivyo Amesema Serikali inaunga mkono juhudi zote za wananchi za kujiletea maendeleo, na kwamba hatua ya wananchi hao kuamua kujenga shule ya Sekondari ya Bweni ,ni jambo la linalopaswa kupongezwa na kila mpenda maendeleo.