Wasafiri wawili kutoka Tanzania wamethibitishwa kuwa na maambukizi ya aina mpya ya virusi vya corona vya Afrika Kusini nchini Denmark.
Kwa mujibu wa mtandao wa runinga ya Taifa ya Denmark, taarifa za wasafiri hao wawili zimechapishwa Jumamosi katika ripoti ya taasisi ya utafiti ya kupambana na magonjwa ya kuambukiza, Statens Serum Institut (SSI) imeeleza Wasafiri hao walipimwa tarehe 19 mwezi Januari.
Wote wamekuwa wakijitenga tangu walipowasili Denmark, kwa mujibu wa ripoti ya SSI. Shirika hilo la Denmark linalsimamia usalama wa wagonjwa limeanzisha mpango madhubuti wa kubaini maambukizi.
Mpaka siku ya Jumapili, jumla ya watu watatu waliokuwa na maambukizi ya aina hiyo ya kirusi walibainika nchini Denmark. Visa vyote vya maambukizi vimehusishwa na safari.
Virusi hivi vya aina ya Afrika Kusini, pamoja na vya Uingereza, vimezua hali ya sintofahamu ulimwenguni. Watu 561 nchini Denmark wamepata maambukizi ya aina hii ya virusi, ambayo pia inaitwa B117, takwimu za SSI zimeonesha siku Jumanne tarehe 19 Januari.
Wakati huo huo, mwishoni mwa wiki iliyopita, serikali ya Uingereza ilitangaza marufuku ya wasafiri kutoka Tanzania na Jamuhuri ya Kidemokrasi ya Congo (DRC) kuingia nchini humo kama sehemu ya mapambano dhidi ya aina hiyo mpya ya virusi vya corona.