Watu wenye bunduki wamelivamia kanisa la kikatoliki katika mji wa Dablo nchini Burkina Faso na kuuwa watu sita jana Jumapili. Kulingana na duru za maafisa wa serikali, waumini walikuwa wakishiriki katika ibda ya asubuhi, wakati walipozingirwa na kundi la wavamizi takriban ishirini walioanza kuwafyatulia risasi. Washambuliaji hao walilichoma kanisa, kisha wakalitia moto duka moja na magari mawili. Mwezi Aprili, wakristo wengine 5 waliuawa katika shambulizi lililolenga kanisa la kiprotestanti katika mji mdogo wa Silgadji pia nchini Burkina Faso, mchungaji akiwa miongoni mwa wahanga. Miji ya Dablo na Silgadji iko Kaskazini mwa Burkina Faso, eneo ambalo limekuwa likiandamwa na mfululizo wa mashambulizi ya umwagaji damu, ambayo inaaminika yanafanywa na makundi ya kigeni yenye itikadi kali, yakiwemo Ansarul Islam, Kundi la Kulinda Waislamu na Uislamu-GSIM, na Dola la Kiislamu katika eneo la Sahara.