Taasisi ya Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu NIMR, imetoa matokeo ya utafiti wa vifo vinavyotokea katika hospitali za Tanzania katika kipindi cha miaka 10 kuanzia mwaka 2006 hadi 2015.
Utafiti huo umeonesha kuwa vifo vya watoto chini ya miaka mitano, vilichangia asilimia 20 ya vifo vyote laki 2 elfu 47 mia 9 na 76, vilivyotolewa taarifa katika kipindi hicho.
Hayo yamesemwa na mtafiti mkuu kiongozi wa taasisi hiyo Dk Leonard Mboera jana, wakati wa ufunguzi wa warsha ya siku mbili ya watafiti wa magonjwa ya binadamu, kutoka taasisi hiyo kuhusu sababu za vifo katika hospitali nchini.
Amesema matokeo ya utafiti huo yameonesha vifo vingi viliathiri kundi la watu wenye umri wa miaka 30-45, ambapo wengi hufa wakiwa na wastani wa umri wa miaka 31 ama kufikia miaka 33 kwa wanaume na wanawake ni miaka 29.
Katika kipindi cha utafiti huo jumla ya vifo laki 2 elfu 47 mia 9 na 76 viliripotiwa, ambako kulikuwa na tofauti kubwa kati ya idadi ya vifo,kwa jinsia ya kiume na ya kike na kwamba vifo vingi viliathiri zaidi wanaume kuliko wanawake.
Vifo vingi vilitokea katika hospitali za mikoa ya Dar es Salaam, Morogoro na Mwanza, ambako vifo katika kundi la watoto nchini ya miaka mitano vilichangia asilimia 20 ya vifo vyote.
Magonjwa yaliyoongoza kusababisha vifo ni malaria, magonjwa ya mfumo wa hewa na Ukimwi.
