Bei ya Mafuta yashuka Nchini.

LICHA ya Serikali kuongeza kodi ya Sh 40 kwa kila lita ya mafuta, bei nchini imeshuka ikilinganishwa na zile za Juni 7 mwaka huu, ambapo kwa sasa bei ya petroli kwa lita imepungua kwa Sh 37, dizeli kwa Sh 14 na mafuta ya taa kwa Sh 19 kwa lita.
Kutokana na hali hiyo, kwa Mkoa wa Dar es Salaam, mafuta ya petroli yatauzwa kwa lita Sh 2,014, mafuta ya dizeli Sh 1,874 na mafuta ya taa Sh 1,806 na kwamba katika Mkoa wa Tanga bei za rejareja za mafuta hayo zimeongezeka huku bei za jumla zikipungua.
Akitangaza bei mpya ya mafuta Dar es Salaam jana, Meneja Mawasiliano na Uhusiano wa Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (Ewura), Titus Kaguo, kwa niaba ya Kaimu Mkurugenzi wa mamlaka hiyo Godwin Samwel, amesema kuwa katika mwaka uliopita wa fedha, kodi ya serikali kwenye mafuta ya petroli kwa lita ilikuwa Sh 339, mafuta ya dizeli Sh 215 na mafuta ya taa Sh 425.
Kaguo   amesema kwa sasa kodi ya mafuta ya petrol, itakuwa ni Sh 379, mafuta ya dizeli Sh 255 na mafuta ya taa Sh 465 kwa lita.
Hata hivyo, Kaguo ametoa onyo kwa wamiliki wa vituo vya mafuta ambao walihodhi kwa ajili ya kupandisha bei mafuta hayo kuanzia leo, kwamba lengo lao halijatimia, kwa kuwa bei zilizotangazwa ndizo zinazotakiwa kuanza kutumika.
Exit mobile version