BIDEN AIPA MSAADA AFRIKA WA DOLA BILIONI 55

Marekani imetangaza msaada wa dola bilioni 55 kwa nchi za Afrika, ndani ya kipindi cha miaka mitatu ijayo.

Tangazo hilo limetolewa wakati rais Joe Biden akijitayarisha kuwa mwenyeji wa viongozi wa nchi za Afrika, kuanzia leo jumanne, hapa Washington DC.

Biden atafanya majadiliano na kundi dogo la viongozi wa Afrika kuhusu chaguzi zitakazofanyika mwaka 2023 na demokrasia barani Afrika.

Mshauri wa usalama wa taifa katika white house Jake Sullivan, amesema kwamba Marekani inaleta raslimali mezani wakati wa kongamano hilo, akiongezea kwamba Marekani ina nia ya dhati kulisaidia bara Afrika kuliko nchi nyingine.

Biden atawakaribisha kwa chakula cha jioni takriban viongozi 50 wa Afrika, ambapo anatarajiwa kutangaza uanachama wa Afrika katika muungano wa nchi 20 tajiri sana duniani.

Biden pia ameahidi kuongoza juhudi za Afrika kuwa na mwanachama wa kudumu katika baraza la usalama la umoja wa mataifa. Biden vile vile atateua mjumbe maalum kufuatilia utekelezaji wa mambo yatakayojadiliwa katika kongamano hilo.

Exit mobile version