Jaji wa Mahakama Kuu, Kanda ya Iringa, Mary Shangali amewataka Mahakimu na wadau wa Mahakama nchini kote kushirikiana kwa pamoja katika kutoa huduma ya haki kwa wananchi.
Jaji Shangali amesema hayo wakati alipokuwa akiongea na Mahakimu wa Mahakama mkoani Njombe baada ya kuhitimisha ziara yake ya kukagua shughuli za Mahakama katika Mahakama za Mwanzo na Wilaya za Njombe, Ludewa na Makete pamoja na Gereza la Ludewa na Makete.
Aidha, Jaji Shangali alibainisha changamoto alizokumbana nazo katika ziara yake ya kukagua shughuli za Mahakama mkoani Njombe kuwa ni tatizo kubwa la usafiri wa kuwachukua Mahabusu kutoka Magerezani na kuwarudisha.
Amesema kuwa changamoto hiyo haiihusu Mahakama moja kwa moja bali ipo chini ya Jeshi la Polisi, kwa kuwa Mahakama na Polisi wote wanafanya kazi kwa kutegemeana changamoto hiyo inaathiri na inaweza kusababisha mlundikano wa mashauri na Mahabusu magerezani kutokana na Wahusika wa kesi kutofikishwa Mahakamani kwa ajili ya kusikiliza kesi zao kwa wakati stahiki.
Aliongeza kuwa, katika ziara hiyo malalamiko mengine yaliyotolewa yaliwahusisha baadhi ya Mahakimu kuwa na tabia ya kutowasikiliza Washitakiwa kwa makini na hatimaye kutoa maamuzi tofauti na uhalisia wa shauri husika.
Aidha; Mhe. Jaji Shangali amesisitiza juu ya utoaji wa Adhabu Mbadala kwa watuhumiwa wenye makosa madogo madogo ili kuepuka mlundikano usio wa lazima magerezani.
