WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema Serikali itaendelea kuchukua hatua kali kwa watu wote watakaothibitika kufanya vitendo vya kuwakatisha watoto wa kike ndoto za masomo ikiwemo kuwafunga jela miaka 30.
Pia amewaagiza Wakuu wa Wilaya wote nchini wahakikishe wanaendelea kushirikiana na Kamati za Ulinzi na Usalama hadi ngazi za kata kusimamia Sheria ya Elimu ya kuwalinda watoto wote wa kike walio chini ya umri wa miaka 18.
Waziri Mkuu ametoa kauli hiyo wakati alipoweka jiwe la msingi na kukabidhiwa shule ya sekondari ya wasichana ya Bunge High School,iliyojengwa na wabunge katika Kata ya Kikombo jijini Dodoma kwa thamani ya zaidi ya sh. bilioni moja.
Amesema utoaji wa elimu bora kwa Watanzania ni moja ya vipaumbele vya nchi katika kuleta maendeleo na kufikia malengo ya Milenia 2025, Elimu kwa wote (EFA) na Mkakati wa Kupambana na Kupunguza Umasikini Tanzania (MKUKUTA).
Waziri Mkuu amesema ili kuweza kufanikisha hayo wanahitaji sekta hiyo iwe bora, imara, inayokidhi mahitaji ya jamii kwa kuwapa vijana maarifa na ujuzi wa kukabiliana na matatizo ya kijamii, kitaifa na kimataifa.
Amesema Serikali kwa kushirikiana na wananchi na wadau mbalimbali imepata mafanikio makubwa sana kwa upatikanaji wa huduma za jamii ikiwemo elimu, afya na maji, ambapo kwa sasa kuna shule za msingi 17,659 na shule za sekondari 4,883 nchi nzima zikiwemo shule za sekondari za Serikali za wasichana 156.
Amesema Serikali, itaendelea kusimamia utekelezaji wa sera ya Elimumsingi Bila Ada kwa lengo la kuwawezesha watoto wa kike kupata elimu ya sekondari na stadi za kazi, kuondoa vikwazo kwa watoto wa kike kupata elimu ya sekondari, kuimarisha matumizi ya TEHAMA katika ufundishaji na ujifunzaji pamoja na uratibu, usimamizi na tathmini ya ubora wa elimu ya sekondari.
Waziri Mkuu amesema Serikali imeweka mikakati maalum ya kuwasaidia watoto wa kwa kuhakikisha wanapata elimu bora na kutokana na mikakati hiyo idadi ya wanafunzi wa kike wanaosoma Elimu ya Juu imekuwa ikiongezeka mwaka hadi mwaka katika ngazi mbalimbali
