Mahakama ya Juu Kenya imeamua uchaguzi wa marudio wa urais uliofanyika tarehe 26 Oktoba, 2017 ulikuwa halali.
Rais Uhuru Kenyatta alitangazwa mshindi wa uchaguzi huo baada ya kiongozi wa upinzani Raila Odinga kususia uchaguzi huo.
Mahakama ya Juu ilikuwa imebatilisha uchaguzi wa kwanza uliokuwa umefanyika tarehe 8 Agosti ambapo Kenyatta alikuwa pia ametangazwa mshindi.
Kenyatta kuapishwa Jumanne kwa muhula wa pili
Rais Kenyatta sasa anatarajia kuapishwa kuwa Rais kwa muhula wa pili baada ya Mahakama ya Juu kufutilia mbali kesi ambazo zilikuwa zinapinga ushindi wake katika uchaguzi wa marudio uliofanyika tarehe 26 Oktoba.
Kifungu 141(1b) cha Katiba ya Kenya kinasema Rais anafaa kuapishwa siku ya saba inayofuata siku ya kutolewa kwa uamuzi wa mahakama wa kuidhinisha uchaguzi iwapo kulikuwa na kesi iliyokuwa imewasilishwa.
Rais kwa mujibu wa katiba anafaa kuapishwa hadharani mbele ya Jjai Mkuu au Naibu Jaji Mkuu.
