Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan , amesema kuwa serikali haitarudi nyuma kamwe katika mapambano dhidi ya rushwa na ufisadi nchini mpaka hapo vitendo hivyo vitakapokoma.
Samia Suluhu ametoa kauli hiyo wakati anafungua Mkutano wa Kimataifa wa ngazi ya Juu, wenye lengo la kubadilishana uzoefu katika mapambano dhidi ya rushwa katika ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Julius Nyerere Jijini Dar es Salaam.
Makamu wa rais ameeleza kuwa vita ya kupambana na vitendo vya rushwa na ufisadi ni kipaumbele cha kwanza ,katika Serikali ya awamu ya Tano na wale wote wanaowezesha, kunufaika na kuhusika na vitendo hivyo wataendelea kuchukuliwa hatua kali za kisheria ili kukomesha vitendo hivyo nchini humo.
Aidha amesema Serikali ya Awamu Tano chini ya Uongozi Shupavu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt John Pombe Magufuli, inaendelea kukaza kamba katika mapambano dhidi ya rushwa ambayo kwa muda mrefu sasa yamechangia kurudisha nyuma, juhudi za Serikali za kuwaletea wananchi maendeleo endelevu.
Amesema Serikali ya Tanzania inalenga kufikia kipato cha kati na kuimarisha uchumi wa viwanda hadi ifikapo mwaka 2025 hivyo malengo hayo yatafanikiwa haraka iwapo tu vitendo vya rushwa vitakomeshwa katika ngazi zote nchini.
