Mufti wa Tanzania awataka watanzania na waislamu wote kulinda amani ya Nchi.

MUFTI wa Tanzania na Shekhe Mkuu wa Tanzania, Abubakar Zubeiry Bin Ally amehimiza umoja, upendo na mshikamano kwa Waislamu na Watanzania kwa ujumla na pia amewataka kulinda Amani ya nchi.

Pia, amesema Baraza Kuu la Waislamu wa Tanzania (Bakwata) lina mipango mikubwa ya kuinua miradi mbalimbali ya maendeleo.

Hali kadhalika, Mufti ameomba viongozi wa dini nchini, kufanya dua ndogo na kubwa katika kuliombea taifa na Rais Dk John Magufuli kwa moyo wa uzalendo katika kuleta maendeleo bila kujali itikadi za dini, siasa na ukabila.

Amesema hayo kwenye Baraza la Idd, lililofanyika kitaifa kwenye msikiti wa Masjid Riadha, mjini Moshi, mkoani Kilimanjaro mara baada ya kuswali sala ya Idd.

Kuhusu maboresho ya uongozi wa Bakwata, Mufti amesema baraza limekuwa imara zaidi kwa kushirikisha taasisi zote za Kiislamu, jambo ambalo linaepusha misuguano isiyo na tija mara kwa mara.

Sherehe hizo zilihudhuriwa na Wajumbe wa Baraza la Ulamaa, Waziri wa Maliasili na Utalii, Prof Jumanne Maghembe, Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Anna Mghwira, IGP mstaafu, Said Mwema, Mbunge wa Moshi Mjini, Jaffary Michael, wakuu wa wilaya za mkoa hwa Kilimanjaro na viongozi mbalimbali wa dini na serikali.

 

 

Exit mobile version