RAIS John Magufuli amesema hatua zinazochukuliwa na Serikali ya Awamu ya Tano zinalenga kuwaletea maendeleo ya kweli wananchi na kujenga taifa linalomwamini Mungu.
Dk Magufuli ameyasema hayo mjini Moshi wakati alipoungana na waumini wa dini ya Kikristo kusali Ibada ya Jumapili ,katika Kanisa la Kiaskofu, Jimbo Katoliki la Moshi, Parokia ya Kristo Mfalme na Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Usharika wa Moshi Mjini, Dayosisi ya Kaskazini mkoani Kilimanjaro.
Akizungumza na waumini wa makanisa hayo, aliwataka Watanzania kwa ujumla kuendeleza amani iliyopo nchini kwa kuwa ndio chachu ya maendeleo.
Aidha amewashukuru waumini wa makanisa hayo mawili na Watanzania kwa ujumla, kwa kusimama pamoja kuliombea Taifa amani iliyowezesha wananchi kupiga kura kwa amani katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015, na kutokana na sala zao Mwenyezi Mungu akamuwezesha kuwa Rais wa Tano wa Tanzania.
Pamoja na hayo, Dk Magufuli ametoa msaada wa mifuko 100 ya saruji ,kusaidia maendeleo ya Kanisa Katoliki na Sh milioni moja kwa kwaya ya kanisa hilo ,ili irekodi nyimbo zake.
Akiwa KKKT, Rais huyo alitoa mifuko 150 ya saruji kwa ajili ya kuchangia maendeleo ya kanisa hilo, na Sh milioni moja kwa kwaya ya Kanisa hilo.
Naye Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Uratibu na Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na wenye Ulemavu, Jenista Mhagama, alimuunga mkono mkono Dk Magufuli kwa kuchangia mifuko 50 ya saruji na Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Said Mecky Sadiki alichangia mifuko 50 ya saruji na Sh 500,000.
