Rais wa zamani wa Marekani George H. Bush afariki dunia

Rais wa zamani wa Marekani George H. W. Bush amefariki dunia akiwa na umri wa miaka 94. Mtoto wake wa kiume George W. Bush ambaye naye aliwahi kuwa rais kati ya mwaka 2001-2009, amethibitisha taarifa za kifo cha baba yake na kusema alikuwa mtu wa haiba ya hali ya juu. Kifo cha Bush kinafuatia kifo cha mke wake Barbara, aliyefariki dunia mwezi Aprili. Rais Donald Trump anayehudhuria mkutano wa viongozi wa G20 nchini Argentina, ametuma salamu za pole na kumsifu kuwa mtu aliyejitoa kwa familia yake na nchi. Salamu za pole pia zimetoka kwa rais wa zamani Barack Obama aliyesema Marekani imepoteza kiongozi mzalendo. George Herbert Walker Bush kutoka Republican, alikuwa rais wa 41 wa Marekani kati ya mwaka 1989-1993, wakati ambao aliiongoza nchi yake katikati mwa matukio muhimu ikiwemo kuanguka kwa ukuta wa Berlin na kuporomoka kwa Muungano wa kisovieti.

Exit mobile version