Rais wa Zanzibar atoa pongezi kwa jeshi la Polisi Tanzania

RAIS wa Zanzibar, Dk Ali Mohamed Shein amelipongeza Jeshi la Polisi Tanzania kwa kuendelea kusimamia vyema amani na utulivu Zanzibar.

Akizungumza na Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini (IGP), Simon Sirro aliyefika Ikulu mjini Zanzibar kujitambulisha rasmi, Shein amesema Jeshi la Polisi limekuwa likifanya kazi kubwa katika kuhakikisha amani na utulivu inaimarishwa na wananchi wanajishughulisha na shughuli zao za kijamii wakiwa salama.

Amesema Jeshi hilo Visiwani Zanzibar limekuwa likitekeleza vema kazi zake na kutoa ushirikiano mzuri, kwa wananchi huku akisisitiza kuwa, ipo haja kuongeza ari hiyo ili lizidi kuitumikia vema jamii.

Rais Shein amesema ana matumaini makubwa kwa uongozi wa IGP Sirro na kumuahidi kuwa ataendelea kushirikiana naye pamoja na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ili Jeshi hilo lizidi kupata maendeleo sambamba na kusimamia vema amani na utulivu.

 

 

Naye IGP Sirro ametoa shukurani kwa Dk Shein na kupongeza kwa ushirikiano mkubwa linaoupata Jeshi hilo ,kutoka kwa wananchi na viongozi wote wa SMZ.

 

IGP Sirro amemhakikishia Dk Shein kuwa hatua za makusudi zitachukuliwa kuhakikisha changamoto zilizopo kwa Jeshi la Polisi Zanzibar, zinapatiwa ufumbuzi sambamba na kusimamia usalama wa barabarani

 

Exit mobile version