Serikali ya awamu ya tano yapanga kufanya nyongeza ya kawaida ya kila mwaka katika mishahara.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli, amesema Serikali ya  Awamu ya tano imepanga kufanya  nyongeza ya kawaida ya kila mwaka katika mishahara yaani Annual increment, ambayo ilikuwa imesimama kwa muda mrefu ikiwa ni pamoja na promosheni.

Rais Magufuli ametoa ahadi hiyo katika Sherehe za siku ya Wafanyakazi duniani zilizofanyika, katika Uwanja wa Chuo cha Ushirika Moshi mkoani Kilimanjaro.

Amesema uamuzi wa Serikali wa kuanza kutoa promosheni unatokana na kukamilika kwa zoezi la uhakiki, wa Wafanyakazi hewa  zaidi ya wafanyakazi elfu tisa mia tisa 32 walibainika kuwa wafanyakazi  hewa.

Aidha, Rais Magufuli amewaonya watumishi ambao wamekuwa wakidanganya umri wa kustaafu, ili waendelee kufanya kazi kwa muda mrefu na kuwa siku zao sasa zimekwisha.

Katika hatua nyingine Rais Magufuli amepiga marufuku uhamisho wa Wafanyakazi, bila kuwalipa stahili zao kutokana na kuwepo na tabia ya kuwahamisha wafanyakazi bila kuzingatia taratibu hasa za malipo ya uhamisho.

Rais Mgufuli amewahakikishia wafanyakazi kuwa Serikali ya awamu ya Tano, itaendelea kuwajali na kuwa  karibu nao katika kutimiza dhana ya utatu ya ushirikiano kati ya Serikali, Wafanyakazi na Waajiri kwa lengo la kuleta maendeleo.

Sherehe za Mei Mosi zilizofanyika katika mkoa wa Kilimanjaro pia zimehudhuriwa na Makamu wa Rais Mhe. Samia Suluhu Hassan, Waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa, Spika wa Bunge Mhe. Job Ndugai, Mawaziri, Manaibu Mawaziri, Wabunge na viongozi mbalimbali wa Chama na Serikali ambapo kauli mbiu inasema,” Uchumi wa Viwanda uzingatie kulinda Haki, Maslahi na Heshima ya Mfanyakazi”.

Exit mobile version