Serikali kupitia Msajili wa Jumuiya za Kiraia, Emmanuel Kihampa, imetangaza kulifutia usajili Kanisa la Ufufuo na Uzima linaloongozwa na Mbunge wa Kawe, Askofu Josephat Gwajima, kuanzia Juni 2, 2025. Hatua hiyo imechukuliwa siku moja baada ya Gwajima kutangaza msimamo wake wa kuendelea kukemea vitendo vya utekaji na watu kupotea.
Kwa mujibu wa taarifa rasmi, kanisa hilo limekiuka Sheria ya Jumuiya Sura ya 337 kwa kutoa mahubiri yenye mwelekeo wa kisiasa na kuonyesha nia ya kuichonganisha Serikali na wananchi, jambo linalotajwa kuhatarisha amani na utulivu wa nchi. Katika barua rasmi ya msajili, Gwajima ametakiwa kusitisha mara moja shughuli zote za kanisa hilo, na nakala ya barua hiyo imetumwa kwa Mkuu wa Jeshi la Polisi, IGP Camillius Wambura.
Wiki moja iliyopita, Askofu Gwajima alizungumza na waandishi wa habari kuhusu vitendo vya utekaji, hali iliyozua upinzani kutoka kwa baadhi ya makada wa CCM. Aidha, jana Juni 1, aliitisha maombi ya siku saba kuanzia leo katika zaidi ya makanisa 2,000 ya Ufufuo na Uzima, kwa ajili ya kuombea haki na amani nchini.