Serikali imesema inajipanga kukabiliana na matumizi mabaya ya mtandao ikiwa ni pamoja na kuwachukulia hatua za kisheria wanaotumia vibaya.
Akizungumza katika majadiliano ya usalama wa mitandao ya kijamii kati ya Tanzania na China, Naibu Waziri wa Wizara wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Injinia Edwin Ngonyani amesema serikali itawachukulia hatua kali wanaotumia vibaya mitandao ya kijamii, wakiwamo wanaotuma ujumbe wenye dhamira ya kuwachafua wengine.
Injinia Ngonyani amesema kuwa Tanzania bado ipo nyuma sana katika usimamizi wa mitandao ya kijamii tofauti na china mbayo imefanikiwa kwa kiasi kikubwa.
Naibu Waziri wa Udhibiti wa mtandao wa China, Ren Xianliang amesema nchi yao imefanikiwa kwa kiwango kikubwa katika kudhibiti matumizi ya usalama wa mtandao, kwa kuwa walianzisha mtandao wao ambao umekua unasaidia kufuatilia masuala ya nchi yao vikiwamo vivutio mbalimbali ambavyo huwashawishi na kutoa hamasa kwa wananchi wengi kuweza kutumia mtandao huo.
Aidha amesema pia china imekuwa ikifanya uhamasishaji kupitia vyombo vya habari kwa kuandaa vipindi maaalum kwa ajili ya kutoa elimu kwa wananchi.
