Shamba la Ccm laporwa,Mkuu wa wilaya aagiza waporaji kuliachia.

Mkuu wa Wilaya ya Mbulu Mkoani Manyara, Chelestino Mofuga, amewaagiza viongozi wa Kijiji cha Maretadu chini, waliopora shamba la CCM kuliachia mara moja, kwani shamba hilo linamilikiwa kihalali na chama hicho.

Akizungumza kwenye mkutano wa wananchi wa kijiji hicho, Mofuga ametoa agizo hilo, baada ya kulalamikiwa na baadhi ya wanachama wa chama hicho, kuporwa shamba lao na uongozi hao.

Amesema kitendo cha serikali ya kijiji hicho kuongozwa na Chadema isiwe kigezo cha kuipora shamba la CCM, ambalo lilipatikana kihalali na kwa muda mrefu kabla chama hicho hakijazaliwa.

Aidha ametoa onyo kali kwa mwananchi yeyote atakayejaribu kuvamia mali za CCM ,kwa sababu serikali ya kijiji chao inaongozwa na Chadema, kwani tabia hiyo itasababisha uvunjifu wa amani kwa wananchi.

Awali, mmoja kati ya wajumbe wa serikali ya kijiji cha Maretadu chini, Gerald Sanka amesema waliamua kurudisha shamba hilo kutoka CCM ,baada ya kubaini kuwa lilipatikana kwa ajili ya wananchi na siyo CCM.

Mmoja kati ya viongozi wa CCM wa eneo hilo Zacharia Natse alimshukuru Mofuga ,kwa kuwarudishia shamba lao ambalo liliporwa na kusababisha mkwaruzano wa viongozi wa vyama hivyo viwili.

 

 

Exit mobile version