Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Angellah J. Kairuki, amezitaka Taasisi za Serikali kuratibu suala la uhamisho wa watumishi wa umma kwa makini pale inapohitajika kufanya hivyo ,Ili kuepuka kero na usumbufu kwa watumishi.
Waziri Kairuki amesema hayo jana katika kikao kazi na Watumishi wa Umma wa Halmashauri ya Manispaa ya Ilala eneo la Segerea, jijini Dar es Salaam.
Mhe. Kairuki amesema uhamisho lazima ufanyike kwa mtumishi wa umma endapo kukiwa na sababu za msingi sana ambapo ameongeza
kuwa imebainika wapo baadhi ya watumishi wa umma wanawasilisha sababu mbalimbali kwa waajiri kuomba kuhama, wakiwa na nia ya kukwepa kukaguliwa sifa zao za elimu.
Waziri Kairuki amesisitiza kuwa uhamisho usifanyike kwa mtumishi ambaye anaonekana kuwa na matatizo.
Kairuki ambaye yupo katika ziara ya kikazi katika mkoa wa Dar es salaam ambapo leo ni siku ya tisa akiwa katika Halmashauri ya Manispaa ya Ilala-Segerea, kwa kukutana na watumishi wa umma wa kada zote katika vikao kazi.
Lengo la kukutana na watumishi wa umma ni kusikiliza malalamiko, ushauri na changamoto zinazowakabili katika maeneo yao ya kazi ili kuweza kuzifanyia kazi na kuleta mabadiliko katika Utumishi wa Umma nchini ili kufikia malengo yaliyopangwa na Serikali.
