BODI ya Wakurugenzi ya Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) imeomba serikali umiliki wa bonde la Mto Pangani ili litumike kuongeza uzalishaji wa umeme hali itakayosaidia kuifanya Tanzania kuwa nchi ya uchumi wa viwanda.
Akizungumza baada ya ziara ya siku moja ya kukagua mtambo wa kuzalisha umeme uliopo eneo ya Mnyuzi wilayani Korogwe katika Mkoa wa Tanga, Mwenyekiti wa Bodi hiyo, Alexander Kiaruzi, alisema kutokana na mitambo ya kuzalisha umeme kufungwa katika bwawa hilo huku kukiwa tayari kuna mamlaka nyingine inayohudumia bonde hilo, himekuwa vigumu kwao katika kuweka malengo ya uzalishaji wa nishati hiyo “Tatizo bonde lina mamlaka mbili; umwagiliaji ni kipaumbele cha kwanza halafu umeme ni kipaumbele cha pili, hivyo changamoto inatokea maji yanapokuwa yamepungua,” alisema.
Changamoto nyingine mwenyekiti huyo alisema ni shughuli za kibinadamu zinazofanywa kandokando ya mto ambazo zimekuwa zikiathiri kina cha bwawa hilo kutokana na uwepo wa tope ndani ya mto.
Meneja Msimamizi wa vituo vya kufua umeme vya Hale, Pangani na Nyumba ya Mungu, Steven Mahenda, alisema uingiaji wa mchanga katika bwawa umesababisha mashine kushindwa kufikia uwezo wake wa uzalishaji na kuharibika mara kwa mara. “Licha ya umeme wa gridi ya taifa kujitosheleza katika uzalishaji, lakini kutokana na sera ya viwanda tunalazimika kuweka mikakati ya kuongeza uzalishaji zaidi kwa ajili ya matumizi ya viwanda,” alisema Mahenda.
Meneja Mwandamizi wa Ufuaji Umeme Tanesco, Steven Manda, alisema moja ya mikakati yao ni kuhakikisha mitambo yote iliyofungwa inafanya kazi kwa ufanisi ili kuwa na umeme wa uhakika. “Tumeanza kufanya matengenezo ya uhakika wa mitambo yetu yote ili kuhakikisha Watanzania wanapata umeme wa uhakika na kutosha,” alisema.