Rais mteule wa Marekani, Joe Biden ameonya kuwa hatua ya Rais Donald Trump kukataa kukubali kushindwa na kuratibu mchakato wa kipindi cha mpito cha kukabidhi madaraka, inaweza kusababisha watu zaidi kufa kwa ugonjwa wa COVID-19. Akizungumza na waandishi habari kwenye jimbo la Delaware, Biden amesema watu wengi huenda wakafa iwapo hakutakuwa na ushirikiano. Serikali ya Trump bado haijamkubali rasmi Biden kama rais mteule, hatua inayomaanisha kuwa Biden na timu yake hawawezi kupata taarifa za kijasusi kuhusu masuala ya usalama wa taifa, vile vile kuwa na mpango wa kusambaza chanjo zinazowezekana za COVID-19. Biden amesema wanapopambana na COVID, wanapaswa kuhakikisha kwamba wafanyabiasha na wafanyakazi wana rasilimali na mwongozo wa kitaifa. Biden na Makamu wa Rais mteule, Kamala Harris pia walifanya mikutano kwa njia ya video na vyama vya wafanyakazi na wakuu wa kampuni mbalimbali.