Rais wa zamani Donald Trump anasema atajisalimisha kwa mamlaka katika jimbo la Georgia siku ya Alhamisi kujibu mashtaka katika kesi inayomtuhumu kwa kupanga njama kinyume cha sheria, ya kugeuza matokeo ya uchaguzi wa urais wa mwaka 2020 katika jimbo hilo.
“Unaweza kuamini? Nitaenda Atlanta, Georgia, siku ya Alhamisi KUKAMATWA,” Trump aliandika kwenye mtandao wake wa kijamii Jumatatu usiku, saa chache baada ya dhamana yake kuwekwa na jaji.
Itakuwa ni mara ya nne kwa Trump kukamatwa tangu Aprili, alipokuwa rais wa kwanza wa zamani katika historia ya Marekani kukabiliwa na mashtaka. Jumatatu alasiri, Jaji mmoja wa Georgia, aliidhinisha dhamana ya dola 200,000 kwa Trump katika kesi hiyo ya ulaghai iliyowasilishwa dhidi yake katika jimbo hilo la kusini mwa Marekani.
Trump na wengine 18 katika kesi hiyo ya kihistoria, wamepewa hadi saa sita mchana siku ya Ijumaa kujisalimisha kwa mamlaka huko Georgia ili kusomewa mashtaka. Shirika la habari la CNN liliripoti Jumatatu usiku kwamba Trump atajisalimisha siku ya Alhamisi.
Mbali na dhamana hiyo, Jaji wa Mahakama ya Kaunti ya Fulton Scott McAfee aliweka masharti kadhaa katika makubaliano yaliyoidhinishwa na waendesha mashtaka na mawakili wa Trump.
“Mshtakiwa hatafanya kitendo chochote cha kumtisha mtu yeyote anayejulikana kwake kuwa mlalamishi au shahidi katika kesi hii au kuzuia utoaji wa haki kwa njia yoyote,” McAfee alisema katika uamuzi wa mahakama wa kurasa tatu.
Alisema vitisho kama hivyo vitajumuisha kuchapisha jumbe za mitandao ya kijamii, au kutuma vitisho kama hivyo vikiwa vimechapishwa na mtu mwingine..
McAfee aliweka dhamana ya dola 100,000 kwa kila mmoja kwa washitakiwa wengine wawili katika kesi hiyo — mawakili wa zamani wa kampeni ya Trump John Eastman na Kenneth Chesebro.
