Wahariri walitaka Jeshi la polisi kuongeza kasi ya kumtafuta Azory Gwanda.

Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) wanaamini kutoweka kwa mwandishi Azory Gwanda wa gazeti la Mwananchi kwa siku 17 sasa ni kwa nia mbaya.

Mwenyekiti ya jukwaa la wahariri Teofile Makunga anasema kama mwandishi huyu angekuwa anashikiliwa na vyombo vya usalama kwa sababu yoyote angetakiwa kuwa amefikishwa mahakamani kufikia sasa.

Mkurugenzi wa gazeti la Mwananchi Francis Nanai ameomba vyombo vya ulinzi na usalama kuzidisha kasi ya kumtafuta mwanahabari huyo ambaye ametoweka kwa zaidi ya siku kumi sasa.

Wahariri wanapanga kufanya maandamano ya kushinikiza kuzidishwa kazi kwa msako huo yatakayoanzia mnazi mmoja hadi makao makuu ya wizara ya mambo ya ndani jijini Dar es Salaam.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa awali na kampuni ya magazeti ya mwananchi, mwanahabari huyo wa kujitegemea alitoweka tarehe 21 Novemba.

Bw Gwanda alikuwa anaishi na kuripoti kutoka mji mdogo uitwao Kibiti, ambao upo kilomita kama 130 hivi kusini mwa Dar es Salaam.

Image captionMagazeti ya mwananchi leo yameongoza na kichwa cha habari #MrudisheniAzory

Bwana Gwanda ni mmoja wa waaandishi wa kwanza kabisa kuripoti kwa kina juu ya mfululizo wa mauwaji yaliyokuwa yakitekelezwa na watu wasiojulikana yaliyowalenga polisi na viongozi wa mji huo.

Mauwaji hayo yaliyotokea miezi kadhaa tu iliyopita yalitia hofu kubwa mjini hapo.

Mke wake Anna Pinoni alisema watu wapatao wanne wakiwa kwenye gari aina ya Toyota Land Cruiser nyeupe walimchukua bwana Gwanda kutoka katikati ya mji huo, mahali ambapo hupendelea kukaa.

Anasema pia aliporudi nyumbani alikuta vitu vimezagaa, ishara kwamba inawezekana waliipekua nyumba yao.

Bw Azory aliwasiliana na ofisi za Mwananchi mara ya mwisho tarehe 20 Novemba kwa majukumu ya kikazi.

Exit mobile version