Wauzaji wa maji wa Mererani watakiwa kushusha bei.

Baraza la Mamlaka ya Mji mdogo wa Mirerani Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara, limewataka wauzaji wa maji wanaosambaza na magari kutoka Mji mdogo wa Boma ng’ombe Wilayani Hai Mkoani Kilimanjaro, kushusha bei ya maji ili wananchi wapate unafuu kwani hivi sasa eneo hilo linafikika kwa urahisi.

Mwenyekiti wa Mamlaka ya Mji mdogo wa Mirerani, Adam Kobelo akizungumza kwenye kikao cha Baraza la Mamlaka ya Mji huo jana, alisema hakuna sababu ya wananchi kuuziwa maji kwa bei ghali ilihali barabara ya Kia-Mirerani hivi sasa ni lami tofauti na awali.

Kobelo alisema jamii inapaswa kuona faida ya kuwepo kwa barabara ya lami hivyo hawatakubali waendelee kuuziwa maji kwa bei ghali.

Alisema wananchi waliwachagua ili wawatetee kwenye masuala mbalimbali ikiwemo hilo la bei ghali ya maji na kwa kupitia nafasi hiyo watalisimamia.

“Maji ni uhai, wakati tunasubiri mradi mkubwa tulioahidiwa na Rais John Magufuli, tunapaswa kutatua hili la sasa la maji kuuzwa kwa bei ghali,” alisema Kobelo.

Mwenyekiti wa mtaa wa Kazamoyo, Albert Siloli alisema wananchi wanapaswa kupata faida ya kuwepo kwa barabara ya lami kwa kuona bei ya maji inashuka.

Siloli alisema awali magari ya kutoka Boma ng’ombe hadi Mirerani walikuwa wanatoza fedha nyingi kwenye maji kutokana na ubovu wa barabara lakini sasa hivi barabara imekuwa ya lami lakini hawajashusha bei.

Mwenyekiti wa Kamati ya Elimu, Afya na Maji, Juma Selemani alisema watawaita wauzaji wa maji wa kwenye magari na matenki wa mji huo ili wateremshe bei ya maji.

Selemani haiwezekani bei ya maji ibaki sh1, 000 kwa lita 20 badala ya kushushwa hadi sh500 ili kuendana na hali halisi ya sasa.

Mkazi wa mji huo Japhari Matimbwa alisema viongozi hao wanapaswa kuhakikisha wanasimama kidete ili bei ya maji iteremke kwani imekuwa kero kwa jamii ya eneo hilo.

“Imefikia hatua watu wanalalamika mno kuhusu maji lakini ufumbuzi haupatikani, tunataka kuona juhudi za viongozi kuhusu hilo,” alisema Matimbwa.

 

Exit mobile version