Tetemeko kubwa la ardhi limesababisha vifo vya takriban watu
280 na wengine wengi kujeruhiwa nchini Afghanistan, kwa
mujibu wa shirika la habari la serikali ya nchi hiyo.
Picha zilizosambazwa kwenye mitandao ya kijamii zimeonesha
watu wakiwa kwenye vitanda vya wagonjwa, vifusi na nyumba
zilizoharibiwa katika jimbo la Paktika mashariki.
Ripoti ya Shirika la Habari la Bakhtar limesema huenda idadi ya
waliofariki ikaongezeka na amedai kuwa zaidi ya watu 600
wamejeruhiwa.
Tetemeko hilo lilipiga takriban kilomita 44 kutoka mji wa
kusini-mashariki wa Khost.
Tetemeko hilo ambalo lilipiga wakati watu wengi wamelala
lilikuwa na ukubwa wa kipimo cha 6.1 katika kina cha kilomita
51, kwa mujibu wa kituo cha Utafiti wa Jiolojia cha Marekani.
Katika kipindi cha miaka 10 iliyopita, zaidi ya watu 7,000
wameuawa katika matetemeko ya ardhi nchini humo, Ofisi ya
Umoja wa Mataifa ya Kuratibu Masuala ya Kibinadamu
inaripoti.
Kuna wastani wa vifo 560 kwa mwaka kutokana na matetemeko
ya ardhi.