Watu wenye silaha wameshambulia ofisi ya mkuu wa mashtaka na kituo cha polisi kwenye mji mkuu wa Jamhuri ya Demokrasi ya Congo Kinshasa na kusababisha wafungwa kadha kutoroka
Afisa mmoja wa polisi ameripotiwa kuuawa na wengine wanne kujeruhiwa katika tukio hilo huku kukiwa na ripoti tofauti kuhusu ni wafungwa wangapi walifanikiwa kutoroka.
Hakimu katika wilaya Matete mashariki mwa mji mkuu Kinshasa ameiambia AFP kuwa watu wenye silaha wasiojulikana walishambulia ofisi ya mahakama siku ya Ijumaa usiku, kuchoma magari kadhaa yaliyokuwa yameegesha katika eneo hilo.
Kwa mujibu wa Redio inayofadhiliwa na Umoja wa Mataifa, Radio Okapi, wafungwa 17 walitoroka, wengi kutoka katika kituo cha polisi.
Aidha Mtandao mmoja wa habari nchini DRC Politico, unasema kuwa washambuliajia walikuwa ni wanachama wa Bunda dia Kongo kundi la kidini lenye mtazamo wa siasa.
Serikali inalishutumu kundi hilo kufuatia shambulizi lililotokea katika gereza kuu la Kinshasa mwezi uliopita ambapo mamia ya wafungwa walitoroka.
