SERIKALI imetangaza kuwa watumishi wa umma 450 wameshinda rufaa, kati ya waombaji 1,050 ambao waliwasilisha rufaa zao katika mamlaka husika baada ya kutajwa katika orodha ya watumishi wenye vyeti feki.
Akizungumza na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam, Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Utawala Bora, Dk Laurian Ndumbaro, amesema serikali iliendesha uhakiki wa vyeti vya kidato cha nne, sita na ualimu ambako watumishi wa umma elfu tisa 9,932 walibainika kukutwa na vyeti feki.
Dk Ndumbaro amesema baada ya kutangazwa kwa orodha hiyo ya watumishi wenye vyeti feki, watumishi elfu moja 1,050 walikata rufaa na watumishi 450 pekee, walishinda rufaa hizo huku watumishi 8,800 wakiridhika na matokeo hayo.
Ndumbaro amesema kuwa rufaa hizo zilizokubaliwa ni kwa watumishi wale waliokuwa wakitumia majina ya waume zao baada ya kuolewa, ambayo yalitofautiana na majina yaliyopo kwenye vyeti na baada ya uhakiki walionekana kama ni vyeti feki.
Aidha, amefafanua kuwa wengine walioshinda rufaa ni wale ambao majina yao ya kidato cha nne yalikuwa tofauti na majina ya kidato cha sita kwa kuwa kidato cha nne hakutumia jina la kati kama kidato cha sita, lakini baada ya kujieleza, wamekubaliwa rufaa na kurejeshwa katika utumishi wa umma.
