Mtu anayeshukiwa kuwa na Ebola amewekwa kizuini katika Hospitali ya Kericho, eneo la Bonde la Ufa kusini-magharibi mwa Kenya.
Mgonjwa huyo, ambaye ni mwanamke anaripotiwa kuwa na dalili zinazowapata wagonjwa wa Ebola.
Maafisa wa afya katika Kaunti ya Kericho wamesema kuwa alifanya safari kutoka Malaba eneo la mpaka kati ya Kenya na Uganda.
Hakuna ripoti yeyote iliyotolewa ya kuwepo kwa ugonjwa wa Ebola, karibu na mpaka wa Malaba,Isipokuwa eneo la Magaharibi mwa Uganda.
Sampuli za damu za mgonjwa huyo zimechukuliwa kwa ajili ya kufanyiwa vipimo.
Matokeo ya awali ya vipimo yanatarajiwa kuwa tayari katika kipindi cha saa 12 mpaka 24.
Idara ya huduma za afya ya kaunti ya Kericho imesema inafuatilia kwa karibu suala hili na inafanya kazi pamoja na serikali kuu, kuhakikisha kuwa hatua madhubuti zinafuatwa kuhakikisha usalama wa kiafya kwa wengine.
Serikali ya Kaunti imeuhakikishia Umma kuwa hospitali ya kaunti ina uwezo na ina vifaa kuhakikisha mgonjwa anatengwa na kuwalinda watumiaji wengine wa hospitali, na imetoa wito kwa watu kuwa watulivu na wenye subira.



