Serikali ya Marekani imewawekea vikwazo maafisa watatu wa tume ya uchaguzi nchini DR Congo pamoja na wale wa serikali ya aliyekuwa rais wa taifa hilo Joseph kabila kwa tuhuma za ufisadi.
Taarifa iliochapishwa katika mtandao wa wizara ya fedha nchini Marekani, inasema kuwa watatu hao walidaiwa kula rushwa ili kuzuia na kuchelewesha maandalizi ya uchaguzi wa haki na ulioshirikisha pande zote.
Watatu hao ni rais wa tume ya uchaguzi nchini DRC Corneille Yobeluo Nangaa (Nangaa), naibu wake Norbert Basengezi Katintima (Katintima), na mwanawe Katintima, Marcellin Basengezi Mukolo (Basengezi), ambaye ni mshauri mkuu katika tume hiyo ya uchaguzi CENI.
Kulingana na taarifa hiyo iliotiwa saini na katibu wa maswala ya ugaidi na intelijensia ya kifedha nchini Marekani Sigal Mandelker, watuhumiwa hao walifanya vitendo ambavyo vilikandamiza mikakati ya kidemokrasia au taasisi zake nchini DRC.



