Korti ya Kimataifa ya Uhalifu yenye makao yake mjini The Hague, ICC imemwachia kwa muda aliyekuwa Makamu Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo Jean-Pierre Bemba, baada ya kumuondolea hatia wiki iliyopita. Kuachiwa huko kwa muda kunafungamana na tuhuma za kuwahonga mashahidi wakati kesi yake ilipokuwa ikisikilizwa mwaka uliopita, ambayo kesi yake ya rufaa itasikilizwa tarehe 4 mwezi ujao wa Julai. Majaji wa mahakama ya ICC walimruhusu kuondoka katika jela ya mahakama hiyo mjini The Hague, ikiwa ataheshimu masharti magumu aliyowekewa. Mojawapo ya masharti hayo ni kuripoti mara moja kwenye vyombo vinavyohusika akitakiwa kufanya hivyo, kutobadilisha anuani yake bila kuiarifu mahakama, na kujizuia kutoa tangazo lolote hadharani. Wakili wa Bemba Peter Haynes amesema mteja wake ananuia kurejea mjini Brussels kujiunga na familia yake iliyoko huko.