Benki ya Dunia imetangaza kuwa inatoa mara moja mikopo ya dola bilioni 12 kwa nchi zinazooendelea, kusaidia kupambana na virusi vya corona ambavyo vimesambaa kutoka China hadi nchi 80 duniani. Rais wa Benki ya Dunia David Malpass amesema lengo ni kutoa msaada wa haraka wa kukabiliana na athari za kiafya na kiuchumi zinazosababishwa na janga la COVID 19. Nchi maskini hazina vifaa vizuri vya kuzuia kusambaa kwa virusi vya ugonjwa huo. Fedha hizo huenda zikatumika katika utanuzi wa mifumo ya afya miongoni mwa mambo mengine. Benki ya Dunia siku za nyuma ilizindua mifuko ya msaada wakati wa majanga kama vile Ebola au Zika.



