Waziri Mkuu wa Ukraine Oleksiy Honcharuk amewasilisha barua yake ya kujiuzulu kwa mara ya pili katika miezi miwili. Wabunge kutoka chama tawala wataamua leo kama watakubali kujiuzulu kwake au la wakati wa kikao maalum. Waziri wa fedha na mambo ya nchi za kigeni huenda pia wakaondolewa katika nyadhifa zao kama sehemu ya mabadiliko ya baraza la mawaziri. Naibu Waziri Mkuu Denys Shmygal anapigiwa upatu kuchukua nafasi ya Honcharuk. Shmygal awali alihudumu kama mkuu wa utawala wa kikanda katika jimbo la magharibi la Ivano-Frankvisk kabla ya kuchukua wadhifa wa naibu waziri mkuu mwezi uliopita. Hakukuwa na kauli ya mara moja kutoka kwa Honcharuk au Rais Volodymyr Zelenskiy. Haijafahamika wazi kilichomfanya Honcharuk kuwasilisha barua ya kujiuzulu kwa mara ya pili.



