Arusha, Tanzania – Kuelekea maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani yanayofanyika kila mwaka Tarehe 8 Machi, Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA) kwa kushirikiana na Chuo cha Uhasibu Arusha (IAA) wameandaa kongamano maalumu litakalofanyika Tarehe 6 Machi. Kongamano hilo linalenga kutoa elimu kwa wanawake kuhusu njia za kujiepusha na matokeo ya matumizi ya dawa za kulevya pamoja na kutoa elimu ya afya ya akili.
Akizungumza na Radio 5, Afisa Ustawi wa Jamii Brenda Richard amesema kongamano hili limepangwa kutokana na uhitaji wa wanawake kupata maarifa ya kutambua hatari zinazohusiana na matumizi ya dawa za kulevya, na jinsi ya kujikinga dhidi ya matatizo ya afya ya akili.
“Kwa wanawake ambao tayari ni watumiaji wa dawa za kulevya, au wale ambao wanashuku kuwa wanashawishika, kongamano hilo litawapa mwanga juu ya hatua za kupata msaada na matibabu yanayofaa,” amesema Brenda Richard.
Zaidi, katika kongamano hilo, wataalamu wa magonjwa ya wanawake pamoja na wadau wa afya ya jamii watashirikiana kutoa elimu kuhusu afya ya akili, na kuzungumzia mikakati ya kusaidia wanawake kurekebisha maisha yao na kuishi kwa afya njema.
Kongamano hilo linatarajiwa kuwa jukwaa muhimu kwa wanawake kujifunza, kushirikiana, na kupata msaada wa kitaalamu kuhusu masuala ya afya, afya ya akili, na kuzuia matumizi ya dawa za kulevya.



