Waziri wa mambo ya nje wa Ujerumani Heiko Maas amesema haitokuwa sahihi kutarajia mabadiliko ya kisera kutoka kwa Rais wa Marekani Donald Trump baada ya uchaguzi wa katikati mwa muhula. Maas amesema katika ujumbe aliouweka kwenye ukurasa wake wa Twitter, kuwa Marekani inasalia kuwa mshirika muhimu zaidi wa Ujerumani nje ya Ulaya, na kwamba wanahitaji kutathmini upya na kufungamamanisha uhusiano wao na Marekani ili kuendeleza ushirika huo. Kwa upande wake, makamu wa rais wa halmashauri kuu ya Umoja wa Ulaya Frans Timmermans, amesifu ushindi wa chama cha Democratic katika uchaguzi huo wa jana, akisema wapiga kura walichagua matumaini dhidi ya hofu, ustaarabu dhidi ya ufidhuli, ujumuishwaji dhidi ya ubaguzi na usawa dhidi ya kutofautisha.Urusi pia imesema haioni kama kutakuwa na mabadiliko yoyote katika uhusiano wa Urusi na Marekani baada ya uchaguzi huo.