Rais wa Halmashauri ya Umoja wa Ulaya Jean-Claude Juncker amepinga mpango wa Uingereza wa kutaka kufanya mazungumzo mapya juu ya mkataba wa nchi hiyo kujiondoa Umoja wa Ulaya. Bwana Juncker pia amesema wasiwasi juu ya Uingereza kuondoka Umoja wa Ulaya bila ya mkataba umezidi kuwa mkubwa. Akiwahutubia wabunge wa Umoja huo mjini Brussels Juncker pia amepinga kufanyika mazungumzo yoyote mapya juu ya mpaka wa Ireland na amesisitiza kuwa mkataba uliokwishafikiwa kati ya Umoja wa Ulaya na Uingereza ndiyo unaofaa zaidi. Waziri wa mambo ya nje wa Ujerumani Heiko Maas amesema mkataba ulioafikiwa ndio unaofaa zaidi na ndio suluhisho la pekee la kuiwezesha Uingereza kuondoka Umoja wa Ulaya. Nchi nyingine za Ulaya pia zimepinga kufanyika mazungumzo mapya juu ya mkataba uliokwishaafikiwa.



