Viongozi wa Jumuia ya Afrika ya Mashariki wamekutana jijini Arusha kaskazini mwa Tanzania, huku kukiwa na hali ya wasiwasi na uadui miongoni mwa nchi wanachama.
Waliowasili Arusha ni mwenyeji Rais John Magufuli wa Tanzania, Paul Kagame wa Rwanda, Yoweri Museveni wa Uganda na Uhuru Kenyatta wa Kenya.
Mwandishi wa BBC Munira Hussein ambaye anafuatilia mkutano huo jijini Arusha anaripoti kuwa Marais wa Burundi na Sudani Kusini wametuma wawakilishi wao kwenye mkutano huo.
Viongozi hao kwa sasa wapo kwenye mkutano wa faragha na wanatarajiwa kutoka saa nane na kuongea na wanahabari.
Katika siku za hivi karibuni Burundi iliitangaza Rwanda kama adui yake. Na kwa upande mwingine Rwanda imekuwa ikilalamikia juu ya kile inachosema vitendo vya utesaji, utekwaji na kurudishwa nyumbani kiholela kwa raia wake wanaosafiri nchini Uganda.
Wanachama wengine wa jumuia hiyo ya EAC ni pamoja na wenyeji wa mkutano Tanzania, Kenya na Sudan ya Kusini.
Sio viongozi wote wa mataifa sita wanachama watahudhuria mkutano huo wa leo. Rais wa Burundi Pierre Nkurunzinza atawakilishwa na naibu wake, wakati Rais wa Sudan kusini Salva Kiir naye atawakilishwa na ujumbe maalum.
Mkutano huu ulipangwa kufanyika Novemba mwaka jana lakini ukaahirishwa mara mbiili baada yab Burundi kuugomea. Burundi inalalamika kwamba jumuia inafumbia macho uhusiano wake mbaya na Rwanda, ambayo kwa sasa ndio nchi adui yake mkubwa katika eneo hili.



